Uvumbuzi wa Isaac Newton Uliosahaulika

 

Isaac Newton, anayejulikana kwa kufanya uvumbuzi wa aina mbalimbali na muhimu katika sayansi, hesabu, na elimu ya anga, kwa kweli, “hufikiriwa na wengi kuwa mwanasayansi mkuu kabisa na mwenye ushawishi wa pekee sana kuliko wote aliyewahi kuishi.” Ukweli usiojulikana sana wa Isaac Newton ni kuhusu ugunduzi wake katika mambo ya dini, ikiwemo imani yake kuwa mfumo wa Ukatoliki wa Rumi ulikuwa ndiyo mamlaka ya mpinga Kristo. Watu wengine wengi mashuhuri walikuwa na mtazamo huohuo kama vile Mfalme James, Martin Luther (Mwanzilishi wa Kanisa la Lutheran), John Calvin (Mwanatheolojia Mashuhuri), John Wycliffe (Profesa wa Chuo Kikuu cha Oxford), Thomas Cranmer (Askofu Mkuu wa Canterbury), John Knox, na wengi sana miongoni mwa wanamatengenezo wa Kiprotestanti.

 

Kwa nini Newton pamoja na watu hawa waliofahamika kuwa na uwezo wa juu kabisa wa kiakili, baadhi yao wakiwa waanzilishi wa makanisa, waamini mambo hayo yasiyovutia kuhusu taasisi ambayo inaendesha vituo vya watoto yatima, shule, hospitali, na waumini ambao ni mfano wa kuigwa kama vile Mama Teresa? Kwa ufupi kabisa, walikielewa kitabu cha Danieli, hasa sura ya saba, kwa namna ambayo wengi wameisahau.

 

Mwelekeo wa Hoja

 

Hivyo ni kitu gani ambacho Isaac Newton na wengine walifahamu kuhusu kitabu cha Danieli ambacho kiliwafikisha kwenye uamuzi kwamba kumpinga Papa? (Zingatia: ili kuelewa aya chache zinazofuata, utatakiwa kusoma taratibu na kwa kutumia Biblia yako.) Hapa kuna ufafanuzi uliorahisishwa zaidi: Danieli sura ya pili na ya saba ni sura zinazoshabihiana ambazo Mungu, kupitia mifano, anatabiri juu ya kuinuka na kuanguka kwa falme nne kubwa za dunia: Babeli, Umedi/Uajemi, Uyunani, na Rumi. Hivi ndivyo mataifa haya yalivyoainishwa: sura ya pili huelezea sanamu yenye aina nne za madini zikiwakilisha falme nne. Kisha Danieli sura ya saba huelezea, si aina nne za madini, bali wanyama wanne wakiwakilisha falme hizohizo huku ikitoa maelezo ya kina zaidi kwa njia ya vielelezo. Kisha katika Danieli 7:20 mwelekeo hubadilika kutoka kwenye mnyama wa nne (Rumi) kwenda kwenye pembe kumi. Hizi huwakilisha nini? Fungu la 24 huonesha kuwa zile pembe kumi huwakilisha wafalme/falme kumi zilizoinuka baada ya na kutoka Rumi. Kwenye hizo pembe 10, chanzo cha Ulaya ya sasa kilitabiriwa.

 

Mwisho, mwelekeo hugeuka na kuhamia kwenye “pembe ndogo” ambayo ndiyo watu hawa wasomi walielewa kuwa mamlaka ya mpinga Kristo (ambayo pia hujulikana kama mfumo Katoliki/Upapa). Mtu fulani anayesoma kijizuu hiki anaweza kufikiri sasa, “Inawezekanaje pembe ndogo inayotajwa katika kitabu cha Danieli kuwa mpinga Kristo? Ni vitu viwili tofauti.” Kwanza, neno “mpinga” katika “mpinga Kristo” humaanisha mambo mawili “kinyume” na “badala ya”: hivyo wanateolojia wengi, wakifahamu hili, wanaelewa neno “mpinga Kristo” kuwa humaanisha watu au taasisi ambazo Biblia huzielezea kuwa zinajidai kutwaa haki za Kristo.

 

Vivyo hivyo, sehemu nyingine ndani ya Biblia ambazo hutumia maneno tofauti kama vile, “mtu wa dhambi,” “mnyama,” “pembe ndogo,” “kahaba mkuu,” zote huwakilisha mamlaka ya mpinga Kristo kwa sababu zimeelezwa kuwa zinajidhihirisha zenyewe kwa njia ya udanganyifu kwamba zina mamlaka ya Kristo. Hivyo Wycliffe anaelezea, “katika sura ya saba ya Danieli, Mpinga Kristo anaelezewa dhahiri kabisa kwa pembe….”

 

Ulinganifu Unaojulikana Sana

 

Pili, hoja ya kina ya fasiri ya watu hawa kimsingi ni kwa sababu sifa za “pembe ndogo” hufanana kama kuinuka na kutawala kwa Ukatoliki. Mifano:

 

1. Fungu la 23, 24—Pembe ndogo huinuka na kutwaa madaraka wakati na baada ya kuanguka kwa Rumi—ndivyo Kanisa Katoliki lilivyoibuka.

 

2. Fungu la 8—Pembe ndogo huinuka toka “miongoni” mwa pembe zingine, ikimaanisha makabila yaliyounda mataifa ya Ulaya—Serikali ya Upapa ilifanya hivyo.

 

3. Fungu la 24—Pembe ndogo inang’oa makundi matatu miongoni mwa makundi makuu kumi ya watu ya awali yaliyoishinda Rumi Magharibi—Ukatoliki uliinuka na kutwaa utawala wa kisiasa kupitia mapigano dhidi ya makabila matatu pinzani ya Aryan: Waheruli, Waostrogothi na Wavandali.

 

4. Fungu la 25—Pembe ndogo huwatesa watakatifu wa Mungu—Makadirio yako katika makumi ya mamilioni ya watu waliouawa katika kipindi cha Mateso ya Kikatoliki ya kukomesha uasi, Vita vya Kidini, na matendo mengine yaliyofanywa na kanisa kwa ushirikiano na serikali. Kitabu cha Kiingereza, “Fox’s Book of Martyrs” hutoa maelezo bayana ya ukatili huo.

 

5. Fungu la 25—Hii pembe ndogo hufikiria kubadili sheria ya Mungu (Amri 10)—Kanisa Katoliki lilibadilisha siku ya pumziko la Sabato toka Jumamosi kwenda Jumapili hivyo kuibadilisha amri ya nne. Makanisa mengi ya Kiprotestanti yamepuuzia badiliko hili lisilo la Kibiblia.

 

6. Kwa maelezo mengi zaidi yanayolinganisha mamlaka haya tembelea www.glowonline.org/dan7

 

Mitazamo Inayopingana na Matengenezo

 

Katika hatua hii mtu fulani anaweza kusema, “Ndiyo, kama tafsiri hii ni kweli, kwa nini basi sijawahi kuisikia kutoka kwa mchungaji au padre wangu?” Kwa kawaida, Kanisa Katoliki halikupenda kunyooshewa kidole kama mamlaka ya mpinga Kristo yanayoelezewa katika Danieli na Ufunuo. Kwa hivyo, majesuiti wao wawili walioitwa Francisco Ribera na Luis de Alcasar walitengeneza njia mbili mbadala za kuutafsiri unabii. Njia hizi za Kikatoliki za kutafsiri zinaitwa “Unabii Uliotimia Zamani” (Preterism) na “Unabii Ujao” (Futurism). “Preterism” huelekeza katika kipindi kilichopita ili kumgundua mpinga Kristo na “Futurism” huelekeza kwa mpinga Kristo asiyejulikana atakayetokea wakati ujao. Jambo la kushangaza, idadi kubwa ya Wakristo wasio Wakatoliki sasa huamini mojawapo kati ya mitazamo hii miwili ya Kikatoliki kuhusu utambulisho wa mpinga Kristo. Hata hivyo, wachache wanafahamu kwamba nguvu ya mpinga Kristo iko hai na inaendelea kutenda kazi hata leo kulingana na Isaac Newton na wengine wengi.

 

Matumizi Binafsi

 

Kwa hiyo suala hili linahusianaje na wewe wakati huu au wakati ujao? Kulingana na fasiri hii mtu fulani anaweza kugundua katika kitabu cha Ufunuo sura ya kumi na tatu kwamba mfumo wa Ukatoliki utarudia matendo yake ya mwanzo ulioyafanya huko Ulaya kwa kiwango kikubwa na kuuongoza ulimwengu katika uamsho wa harakati za kidini ambapo mifumo ya ibada za Kikatoliki zitalazimishwa kwa watu wasiotaka kuifuata. Lakini mnyama/pembe ndogo/Kanisa Katoliki litapataje nguvu kama hiyo? Kama namna ileile ambavyo Kanisa Katoliki lilifanya katika wakati uliopita—kupitia serikali za kisiasa zisizo za dini. Japo jeshi lake ni dogo, Vatikan imekuwa ikifanya kazi kupitia serikali za mataifa mengine ili kutimiza matakwa yake. Inashangaza hata leo, mafundisho ya msingi ya Kikatoliki bado yanadai kuwa kanisa na serikali vinapaswa kuungana ili kulazimisha dini kwa raia.

 

Kwa kuhitimisha, hebu tufikirie Mwokozi wetu aliyewaombea maadui zake. Kinyume chake, historia hakika inaonesha kwamba mfumo wa Ukatoliki uliwaangamiza watu wengi sana kupitia mateso. Mwokozi wetu alifundisha kuwa imani katika Yeye pekee ndiyo iokoayo. Ukatoliki ulifundisha na bado unafundisha kuwa kutoa kiasi fulani cha fedha kunaweza kutuweka huru kutokana na adhabu ya dhambi. Yesu alitutia moyo tusome na kuielewa Biblia sisi wenyewe. Ukatoliki ulizuia Biblia na usomaji wake kwa karne nyingi. Yesu alidai kuwa sawa na Mungu. Ukatoliki ulidai kuwa Papa ni Mungu hasa. Yesu alisema ufalme Wake haukuwa wa ulimwengu huu. Ukatoliki ulikuwa na bado una ajenda za kisiasa. Yesu alitunza amri za Baba Yake. Ukatoliki ulibadili amri 10 za Mungu. Ni dhahiri, sifa hizi na zingine za upinga-Kristo pekee hazikuwaongoza wasomi wengi kuamini kuwa Ukatoliki ulikuwa ndio hasa mpinga Kristo. Badala yake, waliamini kuwa kitabu cha Kristo—Biblia—iliangaza nuru kuhusiana na mfumo huu. Hivyo inaonekana kuwa uelewa wao juu ya mpinga Kristo haukujikita katika mwonekano wa kanisa ubadilikao mbele ya umma, bali juu ya Maandiko yasiyobadilika. Kama watu hawa walikuwa sahihi, basi, ufunuo huu wa matendo ya siku zijazo ya Ukatoliki utathibitishwa, wakati ambapo tungelifanya vyema kusikia wito wa huruma wa Yesu kwa waaminifu waliodanganyika ndani ya Ukatoliki: “Tokeni kwake enyi watu wangu…” Je, Isaac Newton, Mfalme James, Martin Luther, John Calvin, na wengine wengi walikuwa sahihi? Kusoma kwako zaidi tu ndiko kutatoa jibu.

 

*Kwa maelezo zaidi tembelea www.glowonline.org/dan7/ 
www.kujifunzabiblia.com